Kumbukumbu La Sheria 17:1-11 Biblia Habari Njema (BHN)

1. “Msimtolee Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, sadaka ya ng'ombe au kondoo mwenye dosari, wala ubaya wowote, maana hilo ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu.

2. “Kama mkisikia kwamba katika mmoja wa miji yenu kuna mwanamume au mwanamke atendaye maovu mbele ya Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, na kuvunja agano lake,

3. naye amekwenda na kuitumikia miungu mingine na kuiabudu, akaabudu hata jua, mwezi au vitu vingine vya mbinguni ambavyo sikuagiza viabudiwe,

4. nanyi mkaambiwa hayo na mkaisikia taarifa hiyo, mtafanya uchunguzi kamili, na kama ni kweli na ni hakika kuwa kitu hiki kiovu kimefanywa katika Israeli,

5. basi, mtoeni mtu huyo nje ya miji na kumpiga mawe mpaka afe.

6. Hata hivyo, atauawa ikiwa kuna ushahidi wa watu wawili au watatu. Asiuawe ikiwa kuna ushahidi wa mtu mmoja tu.

7. Wale mashahidi ndio watakaoanza kumpiga mawe kwanza, halafu wengine nao wampige mawe. Ndivyo mtakavyokomesha uovu miongoni mwenu.

8. Inawezekana kukatokea mashtaka mengine yaliyo magumu mijini mwenu, kama vile kesi zihusuzo: Unajisi, mambo ya haki za watu, na madhara ya mwili. Ikitokea hivyo, mtaondoka na kwenda mahali alipopachagua Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu,

9. na huko mtawaendea makuhani Walawi, na mwamuzi aliye kazini wakati huo, nanyi mtatoa mashtaka mbele yao, nao watatoa uamuzi wao.

10. Kisha mtafanya kama watakavyowatangazieni pale mahali Bwana atakapopachagua; mtakuwa waangalifu kufanya yote kama watakavyowaagiza.

11. Itawabidi kufanya kufuatana na maongozi watakayowapatia na uamuzi watakaoutoa kwenu. Msiache kutimiza kwa dhati hukumu watakayowatangazia.

Kumbukumbu La Sheria 17