15. Mose akamchinja huyo ng'ombe, akachukua damu akazipaka pembe za madhabahu pande zote kwa kidole chake kuitakasa. Kisha akachukua damu iliyobaki akaimwaga chini kwenye tako la madhabahu ambayo aliweka wakfu kwa kuifanyia ibada ya upatanisho.
16. Kisha, akachukua mafuta yote yaliyokuwa kwenye matumbo yake, sehemu bora ya ini pamoja na figo zote mbili na mafuta yake na kuviteketeza juu ya madhabahu.
17. Lakini nyama ya ng'ombe huyo, ngozi yake na mavi yake, akaviteketeza kwa moto nje ya kambi kama alivyoamriwa na Mwenyezi-Mungu.
18. Kisha, Mose akamleta kondoo dume wa sadaka ya kuteketezwa. Aroni na wanawe wakaweka mikono yao juu ya kichwa cha kondoo huyo.
19. Mose akamchinja na damu ya kondoo huyo akairashia madhabahu pande zake zote.
20. Alimkata huyo kondoo vipandevipande, akaviteketeza pamoja na kichwa chake na mafuta yake.
21. Baada ya matumbo na miguu kuoshwa kwa maji, Mose aliviteketeza vyote juu ya madhabahu pamoja na sehemu nyingine za huyo kondoo kama sadaka ya kuteketezwa. Hiyo ni sadaka itolewayo kwa moto, yenye harufu ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu. Mose alifanya kama alivyoamriwa na Mwenyezi-Mungu.
22. Kisha akamleta kondoo dume mwingine, kwa ajili ya kuweka wakfu. Aroni na wanawe wakaweka mikono yao juu ya kichwa cha kondoo huyo.
23. Mose akamchinja. Akachukua damu ya kondoo huyo na kumpaka Aroni kwenye ncha ya sikio lake la kulia, kidole gumba cha mkono wake wa kulia na cha mguu wake wa kulia.
24. Wanawe Aroni nao wakaja, naye Mose akawapaka kiasi cha damu kwenye ncha za masikio yao ya kulia, vidole gumba vya mikono yao ya kulia na kwenye vidole gumba vya miguu yao ya kulia. Damu nyingine akainyunyizia madhabahu pande zake zote.
25. Kisha, akachukua mafuta yote, mkia pamoja na mafuta yake, mafuta yote yanayofunika matumbo, sehemu bora ya ini, pamoja na figo zote mbili, mafuta yake na paja la mguu wa kulia wa nyuma wa huyo kondoo dume.
26. Kisha, kwenye kile kikapu cha mikate iliyowekwa mbele ya Mwenyezi-Mungu akatoa mkate mmoja usiotiwa chachu, mkate mmoja wenye mafuta na mkate mmoja mdogo, akaviweka vyote juu ya vipande vya mafuta na ule mguu.
27. Mose akaviweka mikononi mwao Aroni na wanawe, nao wakafanya ishara ya kumtolea Mwenyezi-Mungu.
28. Kisha Mose akavichukua vitu hivyo vyote kutoka mikononi mwao na kuviteketeza juu ya madhabahu pamoja na sadaka ya kuteketezwa. Hii ni sadaka ya kuwekwa wakfu, yenye harufu ya kumpendeza Mwenyezi-Mungu; ni sadaka itolewayo kwa moto.
29. Kisha Mose akachukua kile kidari na kufanya ishara ya kumtolea Mwenyezi-Mungu. Sehemu hiyo ya yule kondoo dume wa kuweka wakfu ni mali yake Mose kama alivyoamriwa na Mwenyezi-Mungu.
30. Halafu Mose akachukua mafuta ya kupaka na damu kutoka madhabahu akamnyunyizia Aroni na wanawe hata na pia mavazi yao. Hivyo Mose akamweka wakfu Aroni na wanawe pamoja na mavazi yao.
31. Mose akamwambia Aroni na wanawe, “Chemsheni ile nyama mbele ya mlango wa hema la mkutano, muile hapo mlangoni pamoja na mkate kutoka katika kikapu chenye sadaka za kuwekea wakfu. Fanyeni kama nilivyoamriwa na Mwenyezi-Mungu, kwamba sehemu hiyo italiwa na Aroni na wanawe.