10. Kuhani atazichukua na kuziteketeza juu ya madhabahu ya kuteketezea sadaka.
11. Lakini ngozi ya huyo ng'ombe, nyama, kichwa, miguu, matumbo na mavi yake,
12. yaani ng'ombe mzima aliyesalia atampeleka na kumteketeza nje ya kambi mahali safi ambapo majivu hutupwa, naye atamchoma kwa moto juu ya kuni; atachomwa moto hapo mahali pa kumwagia majivu.
13. “Iwapo jumuiya yote nzima ya Israeli imetenda dhambi bila ya kukusudia kwa kufanya kitu kilichokatazwa na amri ya Mwenyezi-Mungu
14. mara dhambi hiyo itakapojulikana, jumuiya yote itatoa fahali mchanga awe sadaka ya kuondoa dhambi. Watamleta kwenye hema la mkutano.
15. Wazee wa jumuiya ya watu wataweka mikono yao juu ya kichwa cha huyo fahali, kisha atachinjwa mbele ya Mwenyezi-Mungu.
16. Yule kuhani aliyeteuliwa rasmi kwa kupakwa mafuta ataleta sehemu ya damu ya huyo fahali ndani ya hema la mkutano.
17. Atachovya kidole chake katika hiyo damu na kuinyunyiza mbele ya pazia mara saba, mbele ya Mwenyezi-Mungu.
18. Kisha, sehemu ya damu atazipaka pembe za madhabahu iliyoko katika hema la mkutano mbele ya Mwenyezi-Mungu. Damu inayobaki ataimwaga chini kwenye tako la madhabahu ya kuteketezea sadaka iliyo karibu na mlango wa hema la mkutano.
19. Mafuta yote ya mnyama huyo atayachukua na kuyateketeza kwenye madhabahu.