Mit. 28:8-25 Swahili Union Version (SUV)

8. Yeye azidishaye mali yake kwa riba na faida,Humkusanyia mtu awahurumiaye maskini.

9. Yeye aligeuzaye sikio lake asiisikie sheria,Hata sala yake ni chukizo.

10. Kila mtu awapotezaye wenye haki katika njia mbaya,Ataanguka katika rima lake mwenyewe;Bali wakamilifu watarithi mema.

11. Mtu tajiri ana hekima machoni pake mwenyewe;Bali maskini mwenye ufahamu humchunguza sana.

12. Wenye haki washindapo, uko utukufu mwingi;Bali waovu waondokapo, watu hujificha.

13. Afichaye dhambi zake hatafanikiwa;Bali yeye aziungamaye na kuziacha atapata rehema.

14. Mwanadamu mwenye kicho yu heri sikuzote;Bali mshupavu wa moyo ataangukia madhara.

15. Kama simba angurumaye, na dubu mwenye njaa;Ndivyo alivyo mtu mbaya awatawalaye maskini.

16. Mkuu aliyepungukiwa na akili huwaonea watu sana;Bali achukiaye kutamani ataongeza siku zake.

17. Aliyelemewa na damu ya mtuAtalikimbilia shimo; wala mtu asimzuie.

18. Aendaye kwa unyofu ataokolewa;Bali mkaidi wa njia zake ataanguka mara.

19. Alimaye shamba lake atakuwa na chakula tele;Bali afuataye mambo ya upuzi atapata umaskini wa kumtosha.

20. Mtu mwaminifu atakuwa na baraka tele;Lakini afanyaye haraka kuwa tajiri hakosi ataadhibiwa.

21. Kupendelea watu si kwema;Wala mtu kuasi kwa ajili ya kipande cha mkate.

22. Mwenye husuda afanya haraka kuwa tajiri;Wala haufikiri uhitaji utakaomjilia.

23. Amkemeaye mwenzake hatimaye atapata kibali;Zaidi ya mtu ajipendekezaye kwa ulimi wake.

24. Aibaye mali ya babaye au mamaye, na kusema, Si kosa;Mwana huyo ni rafiki wa mtu mharibifu.

25. Mwenye nafsi ya kutamani huchochea fitina;Bali amtumainiye BWANA atawandishwa.

Mit. 28