5. Kila mwenye kiburi ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu;hakika mtu wa namna hiyo hataacha kuadhibiwa.
6. Kwa utii na uaminifu mtu huondolewa dhambi,kwa kumcha Mwenyezi-Mungu huepuka uovu.
7. Mwenyezi-Mungu akipendezwa na mwenendo wa mtu,huwageuza hata adui zake kuwa marafiki.
8. Afadhali mali kidogo kwa uadilifu,kuliko mapato mengi kwa udhalimu.
9. Mtu aweza kufanya mipango yake,lakini Mwenyezi-Mungu huongoza hatua zake.
10. Mfalme huamua kwa maongozi ya Mungu;anapotoa hukumu hakosei.
11. Mwenyezi-Mungu hutaka kipimo na mizani halali;mawe yote mfukoni ya kupimia ni kazi yake.
12. Ni chukizo kubwa wafalme kutenda uovu,maana msingi wa mamlaka yao ni haki.
13. Mfalme hupendelea mtu asemaye kwa unyofu;humpenda mtu asemaye ukweli.
14. Hasira ya mfalme ni kama mjumbe wa kifo;mtu mwenye busara ataituliza.
15. Uso wa mfalme ukingaa kuna uhai;wema wake ni kama wingu la masika.
16. Kupata hekima ni bora kuliko dhahabu;kupata akili ni chaguo bora kuliko fedha.
17. Njia ya wanyofu huepukana na uovu;anayechunga njia yake huhifadhi maisha yake.
18. Kiburi hutangulia maangamizi;majivuno hutangulia maanguko.
19. Afadhali kuwa mnyenyekevu na kuwa maskini,kuliko kugawana nyara na wenye kiburi.
20. Anayezingatia mafundisho atafanikiwa;heri mtu yule anayemtumainia Mwenyezi-Mungu.
21. Mwenye hekima moyoni huitwa mwenye akili;neno la kupendeza huwavutia watu.
22. Hekima ni chemchemi ya uhai kwake aliye nayo,bali upumbavu ni adhabu ya wapumbavu.
23. Moyo wa mwenye hekima humwezesha kusema kwa busara;huyafanya maneno yake yawe ya kuvutia.