Hesabu 3:20-37 Biblia Habari Njema (BHN)

20. Wana wa Merari kwa kufuata familia zao: Mahli na Mushi. Hizi zilikuwa jamaa za Walawi kulingana na koo zao.

21. Familia za Walibni na Washimei zilitokana na Gershoni; hizi ndizo zilizokuwa jamaa za Wagershoni.

22. Idadi yao kwa kadiri ya hesabu ya wanaume wote kuanzia waliokuwa na mwezi mmoja na zaidi ni 7,500.

23. Familia za Wagershoni, iliwapasa kupiga kambi yao upande wa magharibi, nyuma ya hema takatifu

24. naye Eliasafu mwana wa Laeli akiwa mkuu wa ukoo wa Wagershoni.

25. Kazi ya wana wa Gershoni ilikuwa kulitunza hema takatifu, hema pamoja na kifuniko chake, pazia la mlango wa hema la mkutano,

26. mapazia ya ua ulioko kati ya hema takatifu na madhabahu, na pazia la mlango wa ua, na kamba zake. Huduma zote zilizohusu vitu hivi zilikuwa zao.

27. Familia za Waamrami, Waishari, Wahebroni na Wauzieli zilitokana na Kohathi; hizi ndizo zilizokuwa jamaa za Wakohathi.

28. Kadiri ya hesabu ya wanaume wote kuanzia wenye umri wa mwezi mmoja na zaidi ilikuwa 8,600, waliohusika na huduma za mahali patakatifu.

29. Familia za wana wa Kohathi zilitakiwa kupiga kambi yao upande wa kusini wa mahali patakatifu,

30. naye Elisafani, akiwa mkuu wa ukoo huo wa familia za Wakohathi.

31. Wajibu wao ulikuwa kulitunza sanduku la agano, meza, kinara cha taa, madhabahu, vyombo wanavyotumia makuhani mahali patakatifu na pazia; huduma zote zilizohusu vitu hivi zilikuwa zao.

32. Naye Eleazari mwana wa kuhani Aroni aliwekwa kuwa mkuu wa wakuu wa Walawi, na msimamizi wa wahudumu wote wa mahali patakatifu.

33. Familia za Wamahli na Wamushi zilitokana na Merari.

34. Hizi ndizo familia za Merari. Idadi yao kadiri ya hesabu ya wanaume wote kuanzia wenye umri wa mwezi mmoja na zaidi ilikuwa watu 6,200.

35. Mkuu wa ukoo wa familia za Merari alikuwa Surieli mwana wa Abihaili; hawa walitakiwa kupiga kambi yao upande wa kaskazini wa hema takatifu.

36. Wao walipewa kazi ya kutunza mbao za hema takatifu, mataruma, nguzo, vitako na vifaa vyote vya kushikilia hema; huduma zote zilizohusu vitu hivi zilikuwa juu yao.

37. Pia walihitajika kutunza nguzo za ua zilizouzunguka na vitako vyake, vigingi na kamba zake.

Hesabu 3