1 Mambo Ya Nyakati 9:17-30 Biblia Habari Njema (BHN)

17. Walinzi wa hekalu wafuatao pia waliishi katika Yerusalemu: Shalumu, Akubu, Talmoni na Ahimani na ndugu zao. Shalumu alikuwa mkuu wao.

18. Hadi kufikia wakati huo, walinzi kutoka katika koo zao ndio waliolinda Lango la mfalme la upande wa mashariki. Hapo awali, walikuwa walinzi wa maingilio ya makambi ya Walawi.

19. Shalumu, mwana wa Kore, mwana wa Ebiasafu, pamoja na ndugu zake wa ukoo wa Kora, walikuwa na wajibu wa kuyatunza maingilio ya hema la mkutano, kama vile walivyokuwa babu zake wakati wa ulinzi wa kambi ya Mwenyezi-Mungu.

20. Finehasi, mwana wa Eleazari, alikuwa msimamizi wao, hapo awali, naye Mwenyezi-Mungu alikuwa pamoja naye.

21. Zekaria mwana wa Meshelemia, pia alikuwa mlinzi wa maingilio ya hema la mkutano.

22. Jumla, watu 212 walichaguliwa kuwa walinzi wa maingilio ya hekalu. Waliandikishwa kulingana na vijiji walimoishi. Mfalme Daudi na Samueli mwonaji ndio waliowathibitisha katika wadhifa huu muhimu.

23. Basi, watu hao na wazawa wao, waliendelea kuyalinda malango ya nyumba ya Mwenyezi-Mungu.

24. Kila upande, yaani mashariki, magharibi, kaskazini na kusini, palikuwa na lango lililokuwa na walinzi.

25. Walinzi hawa walisaidiwa na ndugu zao waliokuwa wakiishi vijijini, ambao walilazimika kushika zamu ya ulinzi kwa muda wa siku saba, mara kwa mara,

26. kwa maana wale walinzi wakuu wanne, ambao walikuwa Walawi, walikuwa na wajibu wa kusimamia vyumba na hazina ya nyumba ya Mungu.

27. Wao waliishi karibu na nyumba ya Mungu kwa sababu ilikuwa ni wajibu wao kuyalinda na kuyafungua malango yake kila siku asubuhi.

28. Baadhi ya Walawi walisimamia vyombo vilivyotumika wakati wa ibada. Walihitajika kuvihesabu wakati vilipotolewa na wakati viliporudishwa.

29. Wengine walichaguliwa kuvisimamia vifaa vya hekalu, na vyombo vyote vitakatifu, na unga safi, divai, mafuta ya zeituni, ubani na manukato.

30. Lakini kazi ya kutayarisha manukato ilifanywa na makuhani.

1 Mambo Ya Nyakati 9